NA
KULWA MZEE
RAIS wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Wallace Karia, anatarajiwa kuwa
shahidi wa mwisho katika kesi ya kutakatisha fedha inayomkabili aliyekuwa anashikilia
wadhifa huo, Jamal Malinzi na wenzake.
Hayo yalibainika jana katika
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, mbele ya Hakimu Mkazi,
Maira Kasonde, wakati kesi hiyo ilipotakiwa kuendelea, lakini ilikwama kwa
sababu Jamhuri hawakuwa na shahidi.
Akiiwakilisha Jamhuri, Wakili wa
Serikali kutoka Takukuru, Leonard Swai, alidai kesi ilikuja kwa ajili ya
kuendelea na ushahidi, lakini hawana shahidi kwa sababu alikuwa anaumwa.
Swai aliomba kesi hiyo iahirishwe
kwa tarehe ya karibu kwa kuendelea na shahidi wa mwisho.
Mahakama ilikubali kuahirisha
hadi Julai 5, mwaka huu, ambapo Jamhuri wanatarajiwa kufunga ushahidi, baada ya
shahidi wa mwisho, Karia kumaliza kutoa ushahidi wake.
Washtakiwa wengine katika kesi
hiyo ni Mhasibu wa TFF, Nsiande Mwanga, Meneja wa Ofisi TFF, Miriam Zayumba na
Katibu wa shirikisho hilo, Selestine Mwesigwa.
Mwingine ni Karani wa TFF, Flora
Rauya ambao kwa pamoja wanakabiliwa na mashitaka 30 katika kesi ya jinai namba
213 ya mwaka 2017.
Washtakiwa wanakabiliwa na
mashtaka mbalimbali yakiwamo ya kula njama, kughushi, kujipatia fedha kwa njia
ya udanganyifu na utakatishaji wa dola za Marekani 173,335.
Malinzi,
Mwesigwa na Nsiande wanaendelea kusota rumande kwa sababu wanakabiliwa na
mashtaka ya utakatishaji fedha ambayo hayana dhamana kwa mujibu wa sheria.
↧